Loading...
Larger font
Smaller font
Copy
Print
Contents

Tumaini la Vizazi Vyote

 - Contents
  • Results
  • Related
  • Featured
No results found for: "".
  • Weighted Relevancy
  • Content Sequence
  • Relevancy
  • Earliest First
  • Latest First
    Larger font
    Smaller font
    Copy
    Print
    Contents

    69 — Dalili za Kuja Kwa Kristo Mara ya Pili

    Maneno ya Kristo kwa makuhani na wakuu “Angalieni nyumba yenu mmeachiwa hali ya ukiwa” (Mathayo 23:38), yaliwatiya hofu sana mioyoni. Swali likaendelea kuwa katika mawazo yao, kuhusu maana ya maneno hayo. Je, inawezekana hili hekalu kuu lililo tukufu wa taifa likabomolewa na kuwa maghofu?TVV 353.1

    Bashiri ya mabaya yatakayoujia Yerusalemu yalitafakariwa na wanafunzi wake pia. Walipokuwa wakitoka pamoja Naye hekaluni walimkumbusha juu ya uzuri wa hekalu na ngome yake. Mawe yaliyojengewa hekalu yalikuwa marumaru ya thamani kuu, na mengine makubwa mno. Sehemu moja ya ukuta ilistahimili shambulio la Nebukadneza, na majeshi yake. Jinsi mafundi walivyolijenga lilifanana kana kwamba mawe yote ni jiwe moja lililobandikwa hapo toka katika machimbo yake.TVV 353.2

    Mwonekano wake machoni pa Kristo ulikuwa mzuri sana, lakini alinena kwa huzuni, Naona hayo yote. Mnaonyesha kuta hizi kwamba ni ngome zisizoweza kubomolewa, lakini, sikilizeni: Siku zinakuja ambapo “halitasalia hapa jiwe juu ya jiwe ambalo halitabomoshwa.” Alipokuwa peke yake, Petro, Yohana, Yakobo na Andrea walimwendea, wakisema: “Tuambie, mambo hayo yatakuwa lini? Nayo ni nini dalili ya kuja kwako, na ya mwisho wa dunia?” Mathayo 24:3. Yesu hakuwajibu kwa njia ya kutenganisha juu ya uharibifu wa Yerusalemu na siku kuu ya kurudi kwake. Alielezea akiyachanganya mambo yote mawili pamoja. Kama angaliwafunulia wanafunzi wake jinsi mambo yajayo yalivyo hasa, wasingaliweza kuyavumilia kuyasikia. Kwa huruma zake, alichanganya matukio hayo mawili, na kuwaacha wanafunzi wenyewe wachanganue maana yake wenyewe. Aliposema mambo kuhusu uharibifu wa Yerusalemu, maneno ya unabii wake yalikwenda mbele hadi siku kuu ile, Bwana atakapoondoka kuwaadhibu walimwengu kwa ajili ya maovu yao. Mazungumzo hayo yote yalitolewa, sio kwa wanafunzi peke yao, ila pia kwa watu wote watakaoishi katika nyakati za matukio ya historia ya mwisho wa ulimwengu.TVV 353.3

    Kristo akawaambia “Angalieni, mtu asiwadanganye. Kwa sababu wengi watakuja kwa jina langu, wakisema, Mimi ni Kristo; nao watadanganya wengi”. Masihi wengi watatokea wakitangaza kuwa wakati wa, ukombozi wa taifa la Wayahudi umekaribia. Hawa watawapotosha watu wengi. Maneno ya Kristo yalitimia. Kati ya kifo cha Yesu na kuzingirwa kwa Yerusalemu masihi wengi walijitokeza. Udanganyifu wa jinsi hiyo utatokea tena.TVV 354.1

    “Nanyi mtasikia habari za vita na matetesi ya vita, angalieni, msitishwe; maana hayo hayana budi kutukia; lakini ule mwisho wa taifa la Kiyahudi wenyewe bado. Kwa maana taifa litaondoka kupigana na taifa, na ufalme kupigana na ufalme; kutakuwa na njaa, na tauni, na matetemeko ya nchi mahali mahali. Hayo yote ndiyo mwanzo wa utungu”. Walimu watafundisha kwamba dalili hizo ni za kuja kwa Masihi. Msidanganyike; dalili watakazosema kuwa ni dalili za kukombolewa katoka utumwani zitakuwa ni za uharibifu wao.TVV 354.2

    “Wakati huo watawasaliti ninyi mpate dhiki nao watawauawa; nanyi mtakuwa watu wa kuchukiwa na mataifa yote kwa ajili ya jina langu. Ndipo wengi watakapojikwaa nao watasalitiana, na kuchukiana.” Wakristo waliteseka katika hayo yote. Wakina Baba na wakina mama waliwasaliti watoto wao, watoto nao wazazi wao. Marafiki waliwapeleka rafiki zao katika baraza kuu la Sanhedrini. Watesaji waliwaua Stefano, Yakobo na Wakristo wengineo.TVV 354.3

    Kwa njia ya watumishi wake Mungu aliwapa, Wayahudi nafasi ya mwisho ya kutubu. Mungu alijidhihirisha mwenyewe kwa njia ya mashahidi wake katika kukamatwa na kuhukumiwa kwao; walakini ingawa ya hayo walihukumiwa kufa, na mahakimu. Kwa kuwaua hivyo Wayahudi walimsulubisha tena Mwana wa Mungu. Hali hiyo itarudiwa tena. Wakuu wataweka sheria ya kuondoa uhuru wa dini. Watadhani kuwa wanaweza kuilazimisha dhamiri ambayo ni Mungu pekee anayepaswa kuitawala Wataendelea na mipango hiyo mpaka watakapofikia ukingo wasioweza kuupita. Mungu ataingilia kati kwa ajili ya watu wake waaminifu wazishikao amri zake.TVV 354.4

    Mateso yatokeapo wengi hujikwaa na kuanguka wakikana imani ile waliyokuwa nayo zamani. Wale watakaoasi wakati wa mateso ili kujisalimisha nafsi: zao, watawashuhudia uongo na kuwasaliti ndugu zao. Kristo ametuonya kwa mambo hayo, tusishituzwe na hali ya ukatili usio kawaida wa wale watakaokataa kweli.TVV 354.5

    Kristo aliwaambia wanafunzi wake namna watakavyoepuka hatari itakayokuja juu ya Yerusalemu. “Lakini, hapo mtakapoona mji wa Yerusalemu umezungukwa na majeshi, ndipo jueni ya kwamba uharibifu wake umekaribia. Ndipo walio katika Uyahudi na wakimbilie milimani, na walio katikati yake wakimbilie nje, na walio katika mashamba wasiuingie.” Onyo hili lilitolewa kusudi lizingatiwe miaka arobaini, baadaye wakati Yerusalemu utakapoharibiwa. Wakristo walikumbuka onyo hilo, na hakuna hata mmoja aliyeangamia mji ulipotekwa.TVV 355.1

    Kristo alisema: “Ombeni, ili kukimbia kwenu kusiwe wakati wa baridi, wala siku ya Sabato.” Yeye aliyeifanya Sabato, hakuitangua. Sabato haikubatili-shwa au kufutwa na kifo chake. Miaka arobaini baada ya kusulibishwa kwake iliendelea kuwa takatifu.TVV 355.2

    Larger font
    Smaller font
    Copy
    Print
    Contents