Loading...
Larger font
Smaller font
Copy
Print
Contents

Tumaini Kuu

 - Contents
  • Results
  • Related
  • Featured
No results found for: "".
  • Weighted Relevancy
  • Content Sequence
  • Relevancy
  • Earliest First
  • Latest First
    Larger font
    Smaller font
    Copy
    Print
    Contents

    Uchapishaji Wapigwa Marufuku

    Francis I alikuwa akifurahia kuwakusanya kwenye baraza lake wasomi kutoka katika kila nchi. Lakini akiwa amepata msukumo wa kutokomeza “uasi wa kidini”, kiongozi huyu wa wasomi alitoa agizo la kupiga marufuku uchapishaji katika nchi yote ya Ufaransa! Francis I anatoa mmoja kati ya mifano mingi katika historia ikionesha ya kwamba ustaarabu wa kisomi siyo kinga dhidi ya kutovumiliana kiimani na mateso.TK 146.1

    Makasisi walidai kuwa tusi lililotolewa dhidi ya Mbingu kwa kulaani misa lisafishwe kwa damu. Januari 2, 1535 ilipangwa kwa ibada hiyo ya kuogofya. Mbele ya kila mlango ulikuwa umewashwa mwenge kwa heshima ya “sakramenti takatifu.” Kabla ya mapambazuko msafara ulikuwa umejipanga kwenye ikulu ya mfalme.TK 146.2

    “Mkate wa Ekaristi Takatifu ulikuwa umebebwa na askofu wa Paris, aliyekuwa amefunikwa kwa kivuli cha nguo cha kupendeza sana...Baada ya Ekaristi Takatifu alifuata mfalme...Francis I, katika siku hiyo hakuwa amevaa taji yake, ama vazi lolote la kitaifa.” 142Wylie, bk. 13, ch. 20. Katika kila madhabahu alikuwa anainama kwa unyenyekevu, siyo kwa sababu ya maovu yaliyokuwa yameuchafua moyo wake, au ile damu isiyo na hatia iliyokuwa imenajisi mikono yake, lakini ati kwa sababu ya “dhambi ya kufisha” ya watu wake waliokuwa wamediriki kulaani misa.TK 146.3

    Kwenye ukumbi mkubwa wa ikulu ya mfalme, mfalme alikuja na maneno yenye kugusa sana, akilaani kwa uchungu “maovu, makufuru, siku ya huzuni na fedheha zilizokuwa zimelipata taifa.” Na alimwomba kila raia aliyekuwa mwaminifu kusaidia kuangamiza kabisa tauni ya “uasi wa kidini” iliyokuwa imetishia kuiharibu Ufaransa. Machozi yalikuwa yamesonga matamshi yake. Na mkutano wote ukalia, kwa nia moja wakitamka “Tutaishi na kufa kwa ajili ya dini Katoliki!” 143D’Aubigne, bk. 4, ch. 12.TK 146.4

    “Neema iletayo wokovu” imefunuliwa, lakini Ufaransa iliyokuwa imemulikwa na mng’ao wake, wao wakaigeuzia upande mwingine,wakichagua giza badala ya nuru. Walikuwa wameuita ubaya wema na wema ubaya, mpaka walipokuwa wahanga wa kujidanganya kwa hiari yao wenyewe. Nuru iliyokuwa iwaokoe kutoka katika udanganyifu, kutoka katika kutoinajisi mioyo yao kwa hatia ya damu, kwa hiari yao walikuwa wameikataa.TK 147.1

    Maandamano yalipangwa tena. “Kwa mbali kidogo majukwaa ya kuchomea watu yalikuwa yamesimamishwa na juu yake Wakristo fulani wa Kiprotestanti walitakiwa wachomwe moto wakiwa hai, na ilikuwa imepangwa ya kwamba kuni ziwashwe mara mfalme atakapokuwa amekaribia, na msafara ulipaswa kusimama kushuhudia adhabu hiyo.” 144Wylie,bk. 13, ch. 21. Kwa upande wao wahanga wa tukio hili walikuwa watulivu bila kuonesha wasiwasi wowote. Walipotakiwa kuikana imani yao, mmoja wao alijibu, “Ninaamini tu kile manabii na mitume walikuwa wanakihubiri, na kile ambacho watakatifu wote walikuwa wanakiamini. Imani yangu inatumaini katika Mungu kupingana na nguvu zote za kuzimu.” 145D’Aubigne, bk. 4, ch. 12.TK 147.2

    Walipofika ikulu, kutano lile la watu lilitawanyika, na mfalme na maaskofu walikwenda kupumzika, wakipongezana ya kwamba kazi ingeendelea mpaka hapo “uasi wa kidini” utakapokuwa umetokomezwa kabisa.TK 147.3

    Injili ya amani ambayo Wafaransa walikuwa wameikataa, kwa hakika ingedhibitiwa kabisa, na matokeo ya kufanya hivyo yangekuwa ya kuogofya sana. Maandamano mengine yalipita kwenye mitaa ya Paris mnamo Januari 21, 1793. “Kwa mara nyingine, mfalme alikuwa mhusika mkuu; tena kulikuwa na ghasia na makelele, tena kilisikika kilio cha wahanga wengine zaidi, tena kulikuwa na majukwaa meusi ya kuchomea watu; tena mandhari ya siku ile ilimalizika kwa mauaji ya kutisha mno, Louis XVI alikuwa anapambana sambamba na walinzi wake wa gereza na wanyongaji wake, mmoja mmoja aliburutwa mbele kwenye kipande cha gogo, na pale walishikiliwa kwa nguvu zote hadi shoka liliposhushwa shingoni na kichwa kilichokuwa kimetenganishwa na kiwiliwili kiliendelea kuruka ruka juu ya jukwaa.” 146Wylie, bk. 13, ch. 21. Karibu na eneo hilo watu wapatao 2800 waliangamia kwa kukatwa vichwa vyao kwenye mashine ya kukatia vichwa vya wahalifu.TK 147.4

    Matengenezo yalikuwa yameupatia ulimwengu Biblia iliyokuwa imefunguliwa. Upendo wa milele uliwafunulia wanadamu kanuni za mbinguni. Wafaransa walipokataa karama ya mbingu, walikuwa wamepanda mbegu ya uharibifu. Kwa sababu kila matokeo yana chanzo chake, utendaji wa kanuni hii isiyoepukika ulipelekea kwenye Mapinduzi na enzi ya hofli kuu.TK 148.1

    Farel mtu jasiri na mwenye juhudi alilazimika kuikimbia nchi aliyozaliwa na kwenda Uswisi. Hata hivyo aliendeleza bidii na mvuto wake kwenye matengenezo nchini kwao Ufaransa. Akisaidiana na wakimbizi wengine, Maandiko ya Wanamatengenezo wa Ujerumani yalitafsiriwa katika lugha ya Kifaransa, pamoja na Biblia ya Kifaransa vilichapishwa kwa wingi. Vitabu hivi viliuzwa kwenye maeneo mbalimbali na kwa wingi na walnjilisti wa vitabu kule Ufaransa.TK 148.2

    Farel alianza kazi yake kule nchini Uswisi kwa kujifanya mwalimu wa shule, huku kwa uangalifu mkubwa akifundisha ukweli wa Biblia. Wengine waliamini lakini makasisi walijitokeza na kuizuia kazi hiyo, watu waliokuwa na imani za kishirikina waliinuka na kuipinga kazi hiyo. “Hiyo haiwezi kuwa Injili ya Kristo,” makasisi walisisitiza, “tunaona kuhubiriwa kwake hakuleti amani, ila vita.” 147Ibid. bk. 14, ch. 3.TK 148.3

    Alikwenda kutoka kijiji hadi kijiji, akivumilia njaa, baridi, na uchovu na kila mahali alikuwa anakabiliwa na hatari kubwa kwa uhai wake. Alikuwa anahubiri sokoni, makanisani na wakati mwingine kwenye mimbari za makanisa ya makao makuu ya dayosisi. Zaidi ya mara moja alipigwa karibu kufa. Bado alikuwa anasonga mbele. Alikuwa anafika miji iliyokuwa ngome ya uPapa mmoja baada ya mwingine akiyafungua malango yake kwa Injili.TK 148.4

    Farel alikuwa na shauku ya kuanzisha kipimo cha Uprotestanti kule Geneva. Endapo mji huu ungeongolewa, ungekuwa kitovu cha Matengenezo nchini Ufaransa, Uswisi, na Italia. Mingi ya miji na vitongoji vilivyokuwa vinauzunguka mji huu vilikuwa vimepokea Injili.TK 149.1

    Aliingia Geneva akiwa na rafiki mmoja. Lakini aliruhusiwa kuhubiri hotuba mbili tu. Makasisi walimwita mbele ya baraza la kanisa, ambalo wao walikuja wakiwa na silaha zilizokuwa zimefichwa ndani ya mavazi yao, huku wamekamia kumuua. Genge la watu wenye hasira lilikuwa limekusanyika kuhakikisha kifo chake iwapo angeponyoka kutoka katika baraza. Hata hivyo, mahakimu na wanajeshi wenye silaha waliokuwepo hapo, waliokoa maisha yake. Alfajiri na mapema siku ilyofuata alisafirishwa kupitia ziwani kwenda mahali pa usalama. Hivyo ndivyo jitihada zake za kwanza za kuihubiri Injili Geneva zilipoishia.TK 149.2

    Kwa ajili ya jaribio lililofuata chombo kingine duni kikichaguliwa- kijana mdogo mwenye mwonekano wa unyenyekevu kiasi kwamba hakuthaminiwa hata na marafiki waliokiri matengenezo. Lakini, mtu wa aina hiyo angefanya nini endapo Farel alikuwa amekataliwa? “Mungu alivichagua vitu dhaifu vya dunia ili aviaibishe vyenye nguvu” 1 Kor. 1:27.TK 149.3

    Larger font
    Smaller font
    Copy
    Print
    Contents