Loading...
Larger font
Smaller font
Copy
Print
Contents

Tumaini Kuu

 - Contents
  • Results
  • Related
  • Featured
No results found for: "".
  • Weighted Relevancy
  • Content Sequence
  • Relevancy
  • Earliest First
  • Latest First
    Larger font
    Smaller font
    Copy
    Print
    Contents

    Ilani za Janga

    Utabiri wote uliokuwa umetolewa na Kristo kuhusu maangamizi ya Yerusalemu ulitimia kikamilifu kabisa. Ishara na maajabu yalitokea. Kwa miaka saba, mtu mmoja alikuwa akizunguka katika mitaa ya Yerusalemu, akitangaza taabu iliyokuwa inakuja. Mtu huyu wa ajabu alifungwa na kupigwa, lakini, dhidi ya matusi na ukatili aliokuwa akitendewa alikuwa anajibu, “Ole, ole wake Yerusalemu!” Aliuawa wakati mji umezingirwa kama alivyokuwa ametabiri.” 1Milman, History of the Jews, Book 13.TK 25.1

    Yerusalemu ilipoangamizwa hakuna Mkristo hata mmoja aliyeangamia. Baada ya Warumi, wakiwa chini ya Cestius kuuzingira mji, Warumi waliondoka bila kutarajiwa wakati dalili zote zilikuwa zinaonesha kuwa ulikuwa wakati mwafaka wa kushambulia. Jenerali huyu wa Kirumi alirudisha majeshi yake nyuma bila sababu yo yote. Ishara iliyokuwa imeahidiwa ilikuwa imetolewa kwa Wakristo waliokuwa wakisubiri. Lk. 21:20,21.TK 25.2

    Matukio yalidhibitiwa ili Wayahudi au Warumi wasiwazuie Wakristo kukimbia. Cestius aliporudi nyuma, Wayahudi walimfuata, na wakati majeshi hayo yanapambana, Wakristo nchini kote waliweza kukimbia bila kusumbuliwa hadi mahali pa usalama, katika mji wa Pela.TK 25.3

    Majeshi ya Wayahudi, yaliyokuwa yakimwandama Cestius na majeshi yake, yalishambulia kutokea nyuma. Warumi walifanikiwa kurudi nyuma kwa shida sana. Wayahudi walirudi Yerusalemu kwa ushindi wakiwa na nyara zao. Hata hivyo hali hii iliiyoonekana kuwa ya mafanikio ilileta madhara zaidi. Ilichochea roho ya upinzani wa kikaidi dhidi ya Warumi, jambo lililoleta shida kwa mji huu uliokuwa hauwezi kuepuka maangamizi.TK 25.4

    Maafa yaliyoukuta mji wa Yerusalemu ulipozingirwa na Tito, yalikuwa ya kutisha. Mji huo ulizingirwa wakati wa Pasaka, ambapo mamilioni ya Wayahudi walikuwa wamekusanyika ndani ya kuta zake. Akiba za chakula zilikuwa zimeharibiwa kutokana na visasi kati ya vikundi vilivyokuwa vinapingana. Sasa athari zote za njaa zilikuwa zinawapata. Watu walitafuna ngozi za mikanda na ndala zao na mifuko ya ngao zao. Wengi walikuwa wanatoka usiku kutafuta mimea ya porini iliyokuwa imeota nje ya mji, ingawa wengi waliuawa kwa mateso ya kikatili. Mara kwa mara wale waliokuwa wanarudi salama walikuwa wananyang’anywa kile walichokuwa wamepata. Wanaume walikuwa wanawapora wake zao, na wanawake walikuwa wanawapora waume zao. Watoto walikwapua chakula midomoni mwa wazazi wao waliokuwa wazee.TK 26.1

    Viongozi wa Kirumi walikuwa wanataka kuwatia hofu Wayahudi ili wasalimu amri. Wafungwa walichapwa mijeledi, wakateswa na kusulubishwa mbele ya ukuta wa mji. Katika bonde la Yehoshafati na Kalvari, misalaba ilisimikwa kwa wingi. Ilikuwa vigumu kupata nafasi ya kupita kati yake. Kwa hiyo, ile laana iliyotamkwa mbele ya kiti cha hukumu cha Pilato ilitimia: “Damu yake na iwe juu yetu, na juu ya watoto wetu.” Mt. 27:25.TK 26.2

    Tito alishtuka alipoona marundo ya miili ikizagaa mabondeni. Akiwa kama ametekewa, alilitazama lile hekalu zuri na kutoa amri kuwa lisiguswe hata jiwe moja la hekalu hilo. Aliwasihi viongozi wa Kiyahudi wasimlazimishe kupanajisi kwa damu mahali hapo patakatifu . Kama wangekwenda kupigania mahali pengine po pote, kusingekuwa na Mrumi wa kunajisi utakatifu wa lile hekalu! Josephus mwenyewe aliwasihi wasalimu amri ili wajiokoe wao, mji wao, na mahali pao pa ibada. Lakini, walimrushia mishale, na kumtukana mpatanishi wao wa mwisho wa kibinadamu. Juhudi za Tito kuliokoa hekalu hazikusaidia Aliyekuwa mkuu kuliko yeye alikuwa amekwisha kutamka kwamba lisingesalia hata jiwe moja juu ya lingine.TK 26.3

    Hatimaye, Tito aliamua kuliteka hekalu kwa nguvu, akiwa amekusudia kuliepusha na uharibifu ikiwezekana. Hata hivyo, maagizo yake yalipuuzwa. Kijinga cha moto kilirushwa na askari mmoja kwenye mwanya uliokuwa kibarazani, na mara vile vyumba vya nyumba takatifu, ambavyo kuta zake zilikuwa zimefunikwa kwa mbao za mkangazi vilishika moto.. Tito aliwahi pale na kuamuru askari wauzime. Maneno yake yalipuuzwa. Kwa hasira askari walitupa vijinga vya moto kwenye vyumba vilivyokuwa ndani ya hekalu na kisha wakawachinja wale waliokuwa wamejificha mle. Damu ikamiminika kwenye ngazi za hekalu kama maji.TK 27.1

    Baada ya kuangamizwa kwa hekalu, mji mzima ulitekwa na Warumi. Viongozi wa Kiyahudi wakaiacha minara yao iliyokuwa haipenyeki. Tito akatangaza kuwa Mungu alikuwa amewatia Wayahudi mikononi mwake; kwani hakuna injini ambazo zingeweza zingeweza kuzishinda ngome za Wayahudi zilizokuwa imara. Mji pamoja na hekalu viliteketezwa hadi kwenye misingi yake, na ardhi vilipokuwa vimejengwa ililimwa “kama shamba lilimwavyo.” Soma Yer. 26:18. Zaidi ya watu milioni waliangamia; waliosalia wakachukuliwa mateka, wakauzwa kama watumwa, wakapelekwa Rumi, wakatupwa waliwe na wanyama wakali katika viwanja michezo, au kutawanyika duniani kote kama wahamiaji wasio na kwao.TK 27.2

    Wayahudi wenyewe, walikuwa wamekijaza kikombe cha kisasi. Katika matatizo yote yaliyofuata baada ya kutawanyika kwao, walikuwa wanavuna mavuno ambayo mikono yao wenyewe ilikuwa imeyapanda. “haya ndiyo maangamizo yako, Ee Israeli ” Hos. 13:9; “maana umeanguka kwa sababu ya uovu wako.” Hos. 14:1. Mara nyingi matatizo yao yanaelezwa kama adhabu kutokana na tamko la moja kwa moja la Mungu. Yule mdanganyifu mkuu huficha yake kwa mji hiyo. Kwa kuwa waliukataa upendo na rehema kutoka mbinguni kwa ukaidi, Wayahudi waisababisha uizo wa Mungu uondolewe kwao.TK 27.3

    Hatuwezi kuelewa ni kwa kiasi gani amani na ulinzi tunaofaidi ulitokana na Kristo. Uwezo wa Mungu unaodhibiti, humzuia mwanadamu kuangukia moja kwa moja katika mikono ya Shetani. Waasi na wasio na shukurani wana sababu kubwa ya kuwa na shukurani kwa ajili ya rehema ya Mungu. Lakini wanadamu wanapovuka mipaka ya uvumilivu wa Mungu, udhibiti huo huondolewa. Mungu huwa hasimami kama mtekelezaji wa hukumu dhidi ya makosa. Huwa anawaacha walioikataa rehema yake wavune walichokipanda. Kila nuru iliyokataliwa ni mbegu iliyopandwa izaayo matunda ya uhakika. Roho wa Mungu akipingwa kwa muda mrefu, hatimaye huondolewa. Hapo huwa hakuna nguvu ya kudhibitii tamaa mbaya za moyo, huwa hakuna ulinzi dhidi ya hiyana na chuki ya Shetani.TK 27.4

    Maangamizi ya Yerusalemu ni onyo kali kwa wote ambao wanapinga ushawishi wa rehema ya Mungu. Unabii wa Mwokozi juu ya adhabu kwa Yerusalemu utatimia tena. Katika hatima ya ule mji mteule, tunaona maangamizi ya ulimwengu ambao umeikataa rehema ya Mungu na kuikanyaga sheria yake. Historia ya dhiki ya wanadamu ambayo ulimwengu umeishuhudia ni ya kutisha. Matokeo ya kuikataa mamlaka ya mbinguni ni ya kutisha. Lakini tukio baya zaidi linaoneshwa katika ufunuo wa mambo yajayo. Roho wa Mungu anayedhibiti atakapoondolewa, asidhibiti tena mlipuko wa hisia za wanadamu na ghadhabu ya kishetani, ulimwengu utaona matokeo ya utawala wa Shetani kuliko ulivyowahi kuona. Siku hiyo, kama ilivyokuwa katika kuharibiwa kwa Yerusalemu, watu wa Mungu wataokolewa. Soma Isaya 4:3; Mathayo 24:30, 31. Kristo atakuja mara ya pili kuwakusanya kwake walio waaminifu wake. “Ndipo itakapoonekana ishara yake Mwana wa Adamu mbinguni; ndipo mataifa yote ya ulimwengu watakapoomboleza, nao watamwona Mwana wa Adamu akija juu ya mawingu ya mbinguni pamoja na nguvu na utukufu mwingi. Naye atawatuma malaika zake pamoja na sauti kuu ya parapanda, nao watawakusanya wateule wake toka pepo nne, toka mwisho huu wa mbingu mpaka mwisho huu.” Mt. 24:30,31.TK 28.1

    Watu wajihadhari wasije wakayapuuza maneno ya Kristo. Kama alivyowaonya wanafunzi wake juu ya kuharibiwa kwa Yerusalemu, ili waweze kukimbia, ndivyo alivyouonya ulimwengu juu ya siku ya maangamizi ya mwisho. Wote wanaotaka wanaweza kuikimbia ghadhabu inayokuja. “Tena, kutakuwa na ishara katika jua, na mwezi, na nyota; na katika nchi dhiki ya mataifa wakishangaa kwa uvumi wa bahari na msukosuko wake.” Luka 21:25. Soma pia Mathayo 24:29; Marko 13:24-26; Ufunuo 6:12-17. “Kesheni basi, ” ndiyo agizo la Kristo. Marko 13:35. Wale watakaotii onyo hilo hawakuwa gizani.TK 28.2

    Dunia haiko tayari kuupokea ujumbe wa wakati huu kama vile Wayahudi walivyokuwa hawako tayari kupokea onyo la Mwokozi juu ya Yerusalemu. Vyo vyote itakavyokuwa, siku ya Mungu itakuja bila kutegemea kwa wasiomcha Mungu. Dunia inapoendelea na mzunguko wake usiobadilika; wakati watu wamezama katika anasa, katika biashara, katika kutafuata pesa; wakati viongozi wa dini wanakuza maendeleo ya dunia na watu wanadanganyika na usalama wa bandia—ndipo, kama mwizi wa usiku wa manane aibavyo katika makazi yasiyo na ulinzi, uharibifu wa ghafla utawajia wasiojali na wasiomcha Mungu, “wala hakika hawataokolewa.” Soma lThe. 5:2-5.TK 29.1

    Larger font
    Smaller font
    Copy
    Print
    Contents